Tuesday, January 29, 2013

Salaam na shukrani wa Wana Muleba






Ndugu zangu wapigakura wa Muleba,

Pokeeni pongezi za kipekee kwa kazi nzuri mliyofanya – kuleta ushindi mnono kwenu, kwa wanamageuzi nchi nzima na kwa chama chenu – Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA).

Ni ninyi, mabibi na mabwana, mlioleta ushindi katika uchaguzi wa vijiji na vitongoji uliopita ambamo mmevuna viti vya vijiji vitano na vitongoji 10.

Haya siyo matokeo yaliyonyesha tu kama mvua ya ghafla; ni matokeo ya mpango mkakati tuliouasisi – ninyi na mimi – hapo 29 Desemba 2012. Ni matunda ya mafunzo ya uongozi tuliyofanya katika kata zote 18 za jimbo tangu Februari 2012. Ni ushahidi kwa ujenzi wa misingi tuliyofanya pamoja katika maeno mbalimbali Muleba Kaskazini tangu Mei 2012; na Desemba 2012 Muleba Kusini.

Huu ni ushahidi mwanana wa kazi za wote ambao tulishirikiana kuandaa Kongamano Kuu la Jimbo na mikutano mikubwa ya hadhara tuliyofanya Septemba 2012 kwenye vituo vya Muhutwe, Kagoma, Kamachumu, Nyakatanga na Izigo. Bali hatukuwa peke yetu.

Makamanda wengi wameshiriki kikamilifu katika kuleta ushindi huu wa aina yake. Naomba kuwataja wachache, kwa niaba ya wengine wote waliokamilisha kazi hii. Kwa leo acha niwataje Salehe Mashaka, Symphorian Nkokerwa, Robert Rwegasira, Pontian Kaganda, Oliva Ishebabi, Medard Karwani, Zamda Salum, Emmanuel Mugalura, Joan Mary Rwegasira, Mzee Pangani, Ismail Bilyomumaisho, Leonigard Bayona na wengine wengi walioshiriki.  

Wapo pia makamanda kutoka nje ya Muleba ambao tulishirikiana kujenga chama hadi hatua hiyo. Wamo Godbless Lema, Alphonce Mawazo, John Heche, Kamanda Upendo, Concesta Rwamulaza, Peter Mweyunge, Renatus Kilongozi, Victor Sherejei, ambao, kwa nyakati tofauti, tuliwaalika jimboni kufanya kazi na waliitikia bila kusita. Ushindi huu ni wao pia kama ulivyo kwa wananchi wote wanaotafuta kukata minyororo ya utawala wa CCM.

Nakumbuka siku moja, ilikuwa Jumamosi, kabla ya kupiga kura, Karwani na Rwegasira mkaharibikiwa pikipiki mara nne mkitoka Ngenge na Bulyakashaju kwenye mkutano wa mwisho wa kampeni. Poleni na hongereni!

Nakumbuka Ijumaa jana yake, katibu wetu wa kata Ngenge –anafahamika kwa jina la “Kakuru” –  alipigwa na kuuawa na watu wasiojulikana. Mungu aiweke roho yake mahali pema peponi.

Katika mazingira ambamo CCM inanyang’anywa vijiji na vitongoji, hata kama ni kimoja; kwetu ni ushindi. Asitokee hata mtu mmoja kudai kwamba ni ushindi wake. Ni wetu sote. Hongereni makamanda. Leo hii, hatuhitaji kufanya utafiti mwingine. Hapana! Tayari tumejua kuwa ushindi utapatikana kwa maandalizi ya umma – ndani ya vyumba vyao; ndani ya nyumba zao, ndani ya vitongoji na mitaa yao; ndani ya vijiji, kata na wilaya zao. Hapa ndio kazi imeanza.

Aluta continua!  

No comments:

My photo
Nimechongwa na mambo haya: Falsafa, Fasihi, Muziki, Habari na Harakati. Sifuati mkumbo. Napenda kuhoji na kudadisi - hulka ya kifalsafa ya kuusaka ukweli - 'UKWELI ULIO UCHI.'